Makamu wa Rais Mhe. Dkt. Philip Mpango amesema suala la utunzaji wa mazingira na mabadiliko ya tabia nchi linapaswa kupewa kipaumbele katika uendelezaji na ukuzaji utalii ili kuepukana na kuvurugika kwa ikolojia na hatari dhidi ya ustawi wa shughuli za utalii.
Dkt.Mpango ametoa wito leo Oktoba 16,2025 wakati akizindua Jengo la Makumbusho ya Eneo la Hifadhi ya Urithi wa Kijiolojia la Ngorongoro – Lengai lililopo Karatu mkoani Arusha na kusisitiza kuwa, kutokana na uharibifu wa mazingira, dunia inashuhudia muingiliano kati ya wanyamapori na binadamu unaopelekea athari kubwa zaidi, vikiwemo vifo na uharibifu wa makazi na mazao.
Aidha, ameitaka Wizara ya Maliasili na Utalii, kupitia Bodi ya Wakurugenzi na Menejimenti ya Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro kuhakikisha miundombinu ya makumbusho hayo inatunzwa na kutumika kama ilivyokusudiwa. Vilevile, amesema ni muhimu kuweka utaratibu mzuri utakaowezesha ukarabati na matengenezo ya mara kwa mara ya miundombinu na mifumo iliyowekwa katika jengo hilo.
Halikadhalika , Makamu wa Rais ameitaka Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro kufanya jitihada za makusudi kushirikisha jamii inayozunguka eneo hilo katika shughuli za uhifadhi wa eneo hilo, zikiwemo mila na tamaduni zake. Pia ametoa wito kwa Watanzania, kujenga utamaduni wa kutembelea vivutio na maeneo ya kihistoria ili kujifunza na kujionea utajiri mkubwa ambao nchi imejaaliwa.
"Ni vema Wizara kwa kushirikiana na Taasisi zake ihakikishe inatoa mafunzo stahiki kwa watumishi watakaohudumu katika eneo hilo ili kuwawezesha kutumia mifumo iliyopo na kutoa huduma kwa ufasaha na ufanisi, kwa kadri itakavyowezekana, mafunzo hayo yashirikishe wadau wa utalii ambao wana mchango katika kuleta wageni watakaokuja kujifunza kupitia utalii wa mambo mbalimbali yaliyopo katika kituo hicho".Amebainisha Dkt.Mpango.
Ameongeza kuwa, mesema Serikali imechukua hatua mbalimbali za makusudi ili kuhakikisha inaboresha huduma za utalii, ikiwemo kutengeneza filamu za Royal Tour na Amazing Tanzania.








Copyright ©2017 Arusha Regional Comissioner's Office. All rights reserved.