*_Amshukuru Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kuchangia mafanikio ya Utalii Arusha*
Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. CPA Amos Gabriel Makalla, ameahidi kuendelea kuimarisha na kukuza sekta ya utalii, kwa kuandaa mpango mkakati wa miaka mitano wakukuza utalii mkoani humo, katika kipindi cha kuelekea kwenye mashindano ya mpira wa miguu Afrika, AFCON 2027.
Akitoa salama za Mkoa wa Arusha, CPA Makalla, mbele ya mgeni rasmi na Makamu wa Rais Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango wakati wa hafla ya Makabidhiano ya Makumbusho ya Urithi wa Historia ya Jiolojia GEO Park - Ngorongoro Lengai, mradi uliojengwa kwa masaada wa Serikali ya China, iliyofanyika leo Oktoba 16, 2025, kwenye eneo la Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro wilayani Karatu.
Amesema kuwa, uwepo wa Makumbusho hiyo ya Geo Park licha ya kuwa ni historia kubwa kwa Tanzania na Arusha, mkoa ambao ni kitovu cha utalii kwa mikoa ya kanda ya kaskakazini, lipo jukumu kubwa la kuhakikisha Serikali inafikia malengo ya kukuza uchumi kupitia zao la utalii nchini.
Amefafanua kuwa malengo makubwa ya mpango mkakati huo ni kukuza uhifadhi na uoto wa asili kwa kuhakikisha Mamlaka ya Ngorongoro inaendelea kutimiza jukumu lake la kwanza la uhifadhi na utunzaji wa mazingira ili kuendelea kuwa na vivutio vya asili vya utalii, kwa kuzingatia kuwa utalii ni zao la uhifadhi.
Hata hivyo, CPA Makalla ametumia fursa hiyo, kutuma salamu za shukrani kwa Mhe. Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kuchangia mafanikio yanayoonekana kwenye sekta ya utalii Arusha, yanayokuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na Serikali kwa ujumla, kupitia filamu za Royal Tour na Amazing Tanzania tamthilia ambazo, zimekuwa chachu na vichocheo vya kuongeza idadi ya watalii wanaofika Arusha.
"Ili kuendelea kukuza utalii mkoani Arusha Mhe.Dkt. Samia, ameridhia ombi la kusimikwa taa kwenye barabara ya kuanzia eneo la Mto wa Mbu- Karatu mpaka geti la kuingia kwenye Hifadhi ya Ngorongoro ili kuongeza usalama, kujenga barabara ya Km 10 kwa kiwango cha lami, barabara zinazoelekea kwenye hoteli za kitalii pamoja na ujenzi wa barabara ya tabaka gumu inayounganisha hifadhi za Ngorongoro na Serengeti.




Hatimiliki ©2018 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Arusha. Haki Zote Zimehifadhiwa